Tafuta katika Blogu Hii

Ijumaa, 26 Julai 2019

WAZIRI MHAGAMA ATOA MAAGIZO KWA VIONGOZI WA SHAMBA LA KATANI LA HASSAN SISAL ESTATE MAKANYA.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu Mhe. Jenista Mhagama ametoa maagizo kwa viongozi wa Shamba la Katani la Hassan Sisal Estate kuhakikisha wanatatua migogoro na wafanyakazi pamoja na kusimamia haki zao ipasavyo.
Waziri Mhagama ametoa maagizo hayo wakati wa ziara yake Wilayani Same alipofanya ziara katika Shamba la Hassan Sisal Estate ikiwa ni utekelezaji wa maagizo ya Waziri Mkuu, Mhe. Kassim Majaliwa kuhusu masuala ya kazi aliyoyatoa Julai 20, 2019 alipotembelea shamba hilo lililopo Mkoani Kilimanjaro, Wilaya ya Same.
Akizungumza na wafanyakazi pamoja na viongozi wa shamba hilo, ameeleza kuwa waajiri wanatakiwa kutekeleza matakwa yote kwa mujibu wa  Sheria za ajira na mahusiano kazini kwa kuzingatia miongozo na kanuni ambayo inasimamia haki,usawa na misingi thabiti kwa wafanyakazi.  
“Tunataka kuona ninyi kama waajiri mnakuwa na vikao vyenye tija na wafanyakazi katika kuleta suluhu ya masuala mbalimbali ya kazi mnatumia njia zilizo halali kuwapatia haki wafanyakazi wenu,” amesema Mhagama
Katika hatua hiyo Mhagama amezitaka kampuni mbili zilizopo katika shamba hilo yaani Unique Consultancy na UPAMI kuhakikisha wanatoa huduma bora kwa wafanyakazi hao, ikiwemo kuwasilisha michango yao kwa wakati kwenye Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF) na Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) ikiwemo kuweka wazi mikataba yao.
 “Malalamiko na Manung’uniko ya wafanyakazi hawa ni mengi, mnatakiwa mnapaswa  n kuyajadili kwa na mkubaliane kwa pamoja namna bora ya kutatua matatizo yanayowakabili na  yatakayojitokeza hususani kwenye mikataba,” amesema Mhagama.
Katika hatua hiyo, Mhe. Mhagama alimuagiza Meneja wa Wakala wa Usalama na Afya Mahala Pa Kazi (OSHA), kufanya kanguzi za mara kwa mara katika shamba hilo na kuangalia kama wafanyakazi wanakabidhiwa vifaa vya kujinginga na madhara kazini (Protective gears) kwa wakati, pamoja na kusimamia zoezi la upimaji afya kwa wafanyakazi  hao.
Akitoa maelekezo kwa Meneja wa Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) Mkoa wa Kilimanjaro, amemtaka kukabidhi kadi za uwanachama kwa wafanyakazi wa shamba hilo na kufuatilia uwasilishaji wa michango yao kutoka kwa waajiri wao.
Sambamba na hilo, Waziri Mhagama ametaka  Afisa Kazi Mfawidhi wa Mkoa wa Kilimanjaro kutembelea shamba hilo na maeneo mengine mbalimbali katika mkoa huo ili kuelimisha wafanyakazi sheria mbalimbali za kazi na ajira zitakazo wawezesha kutambua haki zao za msingi.
Aidha, Waziri Mhagama alitoa maelekezo juu ya uwepo wa vyama vya wafanyakazi kwenye mashamba yote ya katani yaliyopo nchini, vitakavyosadia kuongeza tija na ufanisi katika shughuli mbalimbali za utendaji kazi.
Pamoja na hayo, Mheshimiwa Mhagama amewataka viongozi wa shamba hilo kuendelea kusimamia vizuri maslahi ya wafanyakazi  ili waweze kuleta tija itakayowapa fursa katika kutekeleza majukumu yao ya kila siku wanapokua kazini.
Naye, Meneja Mshauri wa Shamba hilo, Bw. Ndekirwa Nnyari ameahidi kufanyia kazi maagizo yote yaliyotolewa ikiwemo kuwa na majadiliano ya mara kwa mara na wafanyakazi kwa itakayowapa munufaa ya pamoja.
Kwa upande wake, Meneja wa Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF), Bw. Victor Luvena amesema kuwa watatekeleza maagizo yaliyotolewa na Mheshimiwa Waziri kwa kuchukua hatua za kisheria kwa wale watakaoshindwa kutekeleza.
Hata hivyo mmoja wa Wafanyakazi wa Shamba hilo, Bi. Cheshi Juma amesema kuwa ujio wa Waziri na wataalamu alioambatana nao utasaidia kuondoa kero za wafanyakazi na kujenga mahusiano mazuri na waajiri wao.
“Tumehamasika sana kuona Serikali yetu ipo pamoja nasi katika kutetea maslahi ya wafanyakazi na kushughulikia kero tulizokuwa tukikabiliana nazo katika maeneo ya kazi,” amesema Cheshi.
 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni