Tafuta katika Blogu Hii

Jumamosi, 13 Aprili 2019

ROMBO NA SIHA KUNUFAIKA NA MIRADI YA HOSPITALI ;DKT.MGWHIRA AHIMIZA USIMAMIZI KWA TIJA.

 
Aliyevaa miwani katika Picha   ni Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro Dkt Anna Mgwhira akiwa ameambatana na jopo la Wataalamu akipata maelekezo ya kina kutoka kwa Mkuu waWilaya ya Rombo Bi.Agness Hokororo kuhusiana na hatua ziliyofikiwa katika ujenzi wa Majengo ya Hospitali hiyo .

Mkuu wa mkoa wa Kilimanjaro Dkt.Anna Mgwhira amewataka viongozi wa serikali Mkoani humo  kujikita zaidi katika kusimamia miradi ya maendeleo  katika ngazi ya Vijiji, Kata,Tarafa na Wilaya hali itakayoleta tija kwa wanachi katika kuzifikia huduma muhimu.
Kiongozi huyo ametoa rai hiyo kufuatia ziara yake ya siku moja iliyolenga kukagua miradi ya ujenzi wa hospitali katika wilaya ya Rombo na Siha mkoani humo ambapo ameonyesha kuridhishwa na hatua mbalimbali zilizofikiwa licha ya kukabiliwa na changamoto mbalimbali.
Akifafanua zaidi Dkt.Mghwira amesema hatua mbalimbali za ujenzi huo zinatokana na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika kutekeleza ilani yake kwa vitendo katika kuhakikisha huduma muhimu zinapatikana katika ngazi ya vijiji,Kata,Tarafa na Wilaya na kuwataka wananchi kuipokea miradi hiyo ambayo imelenga kuwasaidia na kuboresha mfumo wa Afya kwa walengwa.
Katika hatua hiyo Mgwhira  amezitaka  mamlaka zilizopewa dhamana ya kusimamia ujenzi wa majengo ya hospitali ya Siha kuongeza kasi kiutendaji katika kuhakikisha wanakamilisha ujenzi huo ndani ya muda uliopangwa na kuwaondolea adha wananchi kuzifikia huduma muhimu za kitabibu.
Kwa upande wake mkuu wa wilaya ya Rombo Bi.Agnes Hokororo amesema ujenzi wa  Hospitali hiyo inayojengwa kwenye kata ya Kirongo Samanga, Kijiji cha Kiwanda Mteri itasaidia wakazi wa eneo hilo sambamba na kuimarisha miundombinu mbalimbali ikiwemo Barabara,Maji na Umeme.
Bw. Frimini Peter ni  mmoja wa wakazi wa eneo hilo ambalo linajengwa hospitali hiyo amesema ni matumaini yao kwamba ujenzi huo ukikamilika utawasaidia kwa kiasi kikubwa na kuwanufaisha kwani wamekua wakizifuata huduma za afya kwa umbali mrefu ,hali inayosababisha wakati mwingine wagonjwa kufia ndani au njiani kwa kukosa uwezo wa kuwafikisha hospitalini.
Ujenzi huo wa hospitali hizo mbili Rombo na Siha kuanza kwake hadi kukamilika kwake utagharimu shilingi billion 3 za kitanzania zilizotolewa na serikali kwa ajili ya kuboresha huduma ya afya kwenye wilaya hizo ambao unatarajiwa kukamilika mwezi june mwaka huu.
Katika Picha hawa ni Mafundi wakitimiza majukumu yao.
Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro Dkt.Anna Mgwhira akishauri jambo kuhusiana na eneo linaloonekana katika moja ya Msingi wa jengo  linalotazamiwa kujengwa na kukamilika siku za usoni katika wilaya ya Rombo.
Aliyenyoosha mkono ni Afisa Mipango Miji wa Mkoa wa Kilimanjaro Bw.Godbless Kimaro akishauri jambo kuhusiana na ujenzi huo.
Aliyenyoosha mkono ni Mkuu wa Wilaya ya Rombo Bi.Agnes Hokororo akitoa ufafanuzi wa kina kwa Mkuu wa Mkoa pamoja na jopo la Wataalam kuhusiana na ujenzi huo. TIZAMA PICHA ZA MAJENGO ZA UJENZI WA HOSPITALI HIYO KATIKA WILAYA YA ROMBO.
PICHA ZIFUATAZO NI HATUA ZA UJENZI ZILIZOFIKIWA KATIKA WILAYA YA SIHA KUTOKANA NA UJENZI HUO.
Moja ya Jengo la Hospitali linalojengwa Wilayani Siha.