Tafuta katika Blogu Hii

Alhamisi, 21 Septemba 2017

MAKALA:SERIKALI YA VIWANDA WALEMAVU WAKIWEZESHWA WANAWEZA MIUNDOMBINU ISIWE KIKWAZO KUKWAMISHA NDOTO ZAO.

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa wakati  akishuhudua mwanafunzi Joseph Mtei ambaye hana mikono yote miwili akiandika kwa kutumia vidole vya miguu  baada kuzindua   Shule ya Sekondari ya ST. Pamachius Inclusive katika kijiji cha Kimashuku wilayani Hai.

Swala la elimu nchini Tanzania Je?walemavu wanahaki sawa ya kupata elimu?  Haki ya kupata elimu kwa wote ni moja ya kauli mbiu inayosadifu maendeleo ya kukua kwa sera na mipango mkakati huru na maendeleo  nchini Tanzania . Je? kuna ukweli gani inayodhihirisha kauli hiyo kwa watu wenye ulemavu?
Watanzania wazalendo  hatuna budi kujiuliza kwa pamoja Je, walimu  wenye dhamana ya kuwafundisha walemavu wana moyo wa upendo na watoto wenye ulemavu?
 Je, vifaa vya mafunzo na vya kufundishia vinakidhi haja na mahitaji ya watoto  hao na Je? kuna fursa sawa ya ushiriki kikamilifu kwa watu wenye ulemavu na wasio na ulemavu?
Shirika lisilo la kiserikali nchini Tanzania Childreach linatumia fursa maalum kuwajali ,kuwathamini na kusimamia ndoto za watoto mbalimbali ikiwemo wenye ulemavu tofautitofauti juu ya haki wajibu na usawa katika  kuwapa  kipau mbele katika elimu ,afya na mahitaji stahki.
 Kufuatia warsha fupi  ya kikao kilicholenga kupokea taarifa ya tathimini ya mradi wa elimu na maendeleo kwa watu wasiosikia (viziwi), Hii inaonekana ni  dhahiri ,shairi kwamba watu wenye ulemavu wanahitaji elimu maalumu licha ya kuwepo na upungufu mkubwa wa walimu wa kufundisha katika shule maalumu hali inayobainishwa kama tatizo na kikwazo kikubwa cha kufikia malengo katika kutimiza ndoto za walemavu.
 Tafiti mbalimbali zinaonyesha  kuwa Serikali inatoa mafunzo kwa idadi ndogo ya walimu wa elimu maalum na kwa wakati mwingine walimu wasiopata mafunzo haya maalum wanachukua jukumu la kutafuta mbinu zenye tija kukamilisha majukumu hayo.
Ukosefu wa walimu unaonekana kuwa ni moja ya sababu inayochangia  umaskini uliokithiri na kusababisha utegemezi wa misaada katika nchi yetu na hata kupelekea ukosefu wa ajira kwa watumishi wenye ulemavu katika nafasi za juu za uongozi.
Matatizo mengi yanalikabili kundi hili kwa kuwalinganisha watu wenye ulemavu na wale wasio na ulemavu na hata kuwakatisha tamaa kwa namna moja au nyingine kutokana na ukosefu wa miundombinu rafiki na vitendea kazi .
 Hii ni wazi kwamba  hali ya umaskini kwa watu wenye ulemavu inaonekana kushamiri kila kuchwapo kutokana  na  kukosekana kwa miundombinu wezeshi hali inaonyesha kutengwa ,kunyanyapaliwa  na kukosa  haki sawa ya kupata elimu japokuwa sera ya elimu nchini Tanzania inatoa haki sawa kwa kila mtu kupata elimu.
Kukosekana kwa haki hii kunadhihirika zaidi kutokana na  idadi ndogo ya miundombinu,Taasisi ikiwemo        shule zinazotoa elimu maalumu ikilinganishwa na haja kubwa ya uhitaji wa walengwa .
Zoezi la utoaji elimu kwa wenye ulemavu wa kutosikia linaonekana katika  sera na miongozo ya elimu kama kivuli hafifu kinachoshindwa kuonesha taswira halisia kutokana na  upungufu wa vitendea kazi.
Upungufu wa vifaa hivyo wezeshi wakati mwingine  unachangia kuzorota kwa msingi imara kwani wakati mwingine katika taasisi hizi muhimu vifaa hivi vinakua havipo  na kama vipo  havikidhi mahitaji kwa walengwa.
Matokeo yake watu wenye ulemavu huchanganywa na wale wanaojiweza na mara nyingi hutegemewa kushindana katika muundo mmoja wenye vigezo vya kielimu.
Hili ni tatizo kubwa katika jamii kwa sababu panapokuwepo na mlemavu wa kusikia anachanganywa na walemavu wengine kama wasiona na wenye mtindio wa ubongo , kitaswira inabidi mwalimu wa wanafunzi  hawa awafundiswe polepole ili waende sambamba na wenye upeo mpana.
Ukweli ni kwamba idadi kubwa ya watu wenye ulemavu wanatoka kwenye familia masikini kutokana na familia nyingi hushindwa kumudu baadhi ya gharama za afya, matibabu na miundombinu wezeshi ambayo itawasaidia kundi hili kujiajiri wenyewe na kumudu shughuli zao za kila siku.
Nchini Tanzania jamii yetu imekuwa katika hitaji kubwa la kupata msaada wa kisheria ikiwemo kuwalinda walemavu huku baadhi ya wazazi/walezi huwachukulia walemavu kama kikwazo na watu wasioweza kushiriki katika kupata elimu na huduma nyingine nyingi za kijamii.
Kumekuwepo na mitazamo tafautitofauti katika jamii ambapo wazazi wa watoto hao wamekua  wakiamini bila elimu walemavu wana nafasi kubwa ya kuishi katika hali ya utajiri kwa maisha yao yote kutokana na kupata misaada midogomidogo na kuwafanya walemavu kuwa kama sehemu ya mradi na kuwa chanzo cha kutokupata elimu itakayo wasaidia kukabiliana na changamoto za kimaisha hasa kiuchumi .
Wakati mwingine‘’Wazazi wana mategemeo kidogo kutoka kwa watoto wenye ulemavu na kuwa na mitazamo kuwa watu wenye ulemavu hawawezi kuelimishwa na muda mwingine wanawaona kama ni dhaifu na mzigo kwao hali inayoongeza unyanyapaa  zaidi katika familia na umaskini unaochangiwa na kipato kidogo au kiwango kidogo cha elimu miongoni mwa familia na kujenga uhalisia wa imani zilizosheheni mila na dhana potofu’’
Hali ya umasikini inachangiwa na miundo mbinu kwa walemavu kutopata huduma sawa katika elimu ,afya na huduma nyingine kwani majengo katika taasisi nyingi hayawaruhusu kuzifikia huduma hizo kwa urahisi mfano ngazi na majengo ya ghorofa.
Katika hatua nyingine inayowafanya walemavu kutopata elimu sawa kama watoto wengine hasa katika sekta ya elimu ni utaratibu wa jinsi ya kujisajili katika shule za kata “walimu wakuu wanavyoandikisha wanafunzi kwa njia ya kupunguza idadi yao.”
Kwa  dhana hiyo watu wenye ulemavu huachwa kwa kisingizio kwamba hakuna waalimu na vifaa kwa ajili ya mahitaji hayo maalumu .
Inaonekana kwamba watu wenye ulemavu wanapochanganywa na wanaojiweza wanafanyiwa mambo yasiyofaa ikiwemo kunyanyanyaswa na kunyanyapaliwa na hatimaye kujiona kama wakati mwingine wanabaguliwa kushiriki  katika shughuli nyingi zilizopo ndani ya mitaala kama michezo na kadhalika. 
 Upungufu mkubwa wa vifaa katika shule za wanafunzi wenye ulemavu  na lugha za alama ndiyo sababu kubwa inayochangia  kutokuwepo kwa usawa wa elimu kwa watu wote .
Matatizo yote haya yanayowakabili watu wenye ulemavu yanachangia kukosa usawa katika elimu na huweza kutatuliwa kwa kuwepo na wataalamu wa kutosha na wenye sifa za kitaaluma pamoja na maslahi tofauti na waalimu wanaofundisha wanafunzi wengine ili kuongeza hamasa  na ari ya kufanya kazi kwa bidii.
Kama ilivyo katika unyanyapaa na ubaguzi kwa misingi ya jinsia ambapo mtoto wa kiume hupewa kipaumbele zaidi kuliko wa kike hali kadhalika mtoto mwenye viungo vyote asiye na ulemavu hupewa nafasi zaidi katika kupata haki kuliko mlemavu hivyo mwandishi wa makala hii anabainisha baadhi ya viashiria na kukosekana kwa haki ya kupata elimu na usawa.
Kama hali hii itaendelea athari za baadae kwa kundi hili linalo nyimwa haki ya elimu na usawa ni umaskini uliokithiri,mateso,chuki,fikra potofu na penginepo utegemezi wa kudumu .
Serikali na mashirika ya kijamii licha ya kuendelea kutoa huduma za ushauri na msada wa kisheria dhidi ya ukatili wadau wanahitajika kufanya kampeni kisaikolojia kuwahamasisha wananchi kuhusiana haki,wajibu na kutatua changamoto za kielimu zinazowakabili watu wenye ulemavu ili kuendana na sera ya taifa nchini Tanzania “serikali ya viwanda” ambapo kupitia shule hizo wanafunzi hao wenyeulemavu wamekua wakifundishwa elimu ya ujasiriamali na kuzalisha bidhaa mbalimbali.
Mbali na kuwepo kwa harakati hizo katika kutimiza majukumu halali kisheria  kwa muktadha wa kukuza na kutambua haki za binaadam jamii inapaswa kutambua kwamba ni watu wenye mahitaji muhimu na ni binadamu kama wengine.
Kusimamiwa kwa sheria za haki za kibinaadam kwa ushiriki sahihi kwa misingi imara katika taasisi muhimu  za kisiasa ,kiuchumi na kijamii zenye dhamana kubwa ya kurahisisha huduma stahiki pamoja na kutoa kipau mbele kwa kundi hili ndio njia pekee ya ukombozi kwa walemavu  kwa kutenga fedha za ujenzi na uboreshaji wa shule maalum kwa ajili ya walemavu na vifaa vya kufundishia  walemavu wasio ona, viziwi, bubu pamoja na wenye utindio wa ubongo kutasaidia kundi hili kustawi na kuondoa dhana ya unyanyapaaji.