Tafuta katika Blogu Hii

Ijumaa, 3 Mei 2019

KILIMANJARO MBIONI KUNUFAIKA KIUCHUMI KUPITIA SEKTA YA MADINI.





Serikali mkoani Kilimanjaro imezindua kituo maalum cha kuuzia madini ya Vito katika wilaya ya Same kitakachosaidia kuleta tija kiuchumi  na kuzuia utoroshaji  wa madini unaofanywa na baadhi ya wachimbaji wadogo wadogo wilayani humo  na wafanyabiashara wa mikoa jirani.
Mkuu wa mkoa  huo, Dk. Anna Mghwira amebainisha hayo katika ziara yake ya kikazi ya siku moja  iliyolenga kujioneo sampuli mbalimbali za madini hayo sambamba na  kukizindua chumba rasmini kitakachotumika kufanyia biashara hiyo kwa muda wakati tafiti za kina zikiendelea .
Akizungumzia swala hilo nyeti mkuu huyo amesema Wilaya ya Same ni miongoni mwa wilaya nne zinazopatikana madini ya vito ikiwemo wilaya ya Mwanga ,Rombo na Siha.
Dk. Mghwira amesema madini mbalimbali ya Vito  pamoja na madini ya ujenzi yanayopatikana mkoani humo yamekua yakisafirishwa na kupelekwa nje ya mkoa huo kwa matumizi tofautitofauti ya viwandani   kwa njia zisizo halali .
“Wilaya hii inapatikana madini mbalimbali kama vito , madini ya ujenzi na madini ya viwandani ambapo wapo wachimbaji wamekuwa wakiyatorosha na kwenda kuyauza nje ya mkoa wetu hivyo kuwepo kwa kituo hicho kutadhibiti biashara hiyo” amesema Dk. Mghwira.
Akifafanua zaidi Dkt.Mgwhira amesema, kituo hicho cha kuuzia madini kitakuwa maalum kwa ajili ya kuuzia madini ya vito yanatopatikana kwa asilimia kubwa katika  ukanda wa milimani  ambapo yataibua   fursa za ajira kwa wazawa kama ilivyo azima ya  Serikali kuwahudumia wananchi wake  na kupanua wigo katika sekta ya  viwanda kwa kuzingatia rasilimali ghafi zilizopo .
Mkuu huyo amesema, uwepo wa kituo hicho cha kuuzia madini kutaamsha hari  hamasa kwa wazawa kuwekeza katika sekta hiyo kisheria ikiwemo kujisajili na kupata leseni itakayowawezesha  kufanya biashara hiyo kwa halali ikiwa ni pamoja na kulipa kodi stahiki ya Serikali.
”Tumekua tukipata hasara pasipo kujua umuhimu wa rasilimali zetu  hivyo sisi kama watendaji inatubidi tuwe macho na kutumia fursa zilizopo kukuza uchumi kwa maslahi ya taifa kwa kuweka mbele uzalendo ,utashi na uwajibikaji bado  serikali inaendelea na mchakato ili kuona umuhimu wa kuanzisha kituo kingine kwa ajili ya kuuzia madini ya ujenzi  ya viwandani”amesema Mgwhira .
Akizitaja fursa zilizopo katika wilaya ya Mwanga amesema kunapatikana madini ya Shaba, Vito na madini ya ujenzi, wilaya ya Rombo yanapatikana  madini ya Pozolana na matofali ya kuchonga ambapo huuzwa nchini Kenya kwa wingi huku wilaya ya Siha kukipatikana madini ya Ujenzi.
Kwa upande mkuu wa wilaya ya Same, Rosemary Senyamule amesema , kufunguliwa kwa kituo hicho kutasaidia kukuza uchumi wa wilaya ya Same na mkoa wa Kilimanjaro kwa ujumla na kukidhi mahitaji ya ziada na kiada kupitia huduma mbalimbali za kijamii ikiwemo afya,elimu,miundombinu stahiki.
Katika hatua hiyo Senyamule ametumia nafasi hiyo kuwataka wachimbaji wadogo wilayani humo  kuchangamkia fursa hiyo kwa kukata leseni za uchimbaji wa madini hayo ya vito ili kuepuka  migogoro mbalimbali isiyo na tija hapo baadae.
Aidha ametoa onyo kwa wachimbaji na wafanyabiashara wialayani humo kuacha mara moja tabia ya kutorosha madini na badala yake wafike katika kituo hicho cha kuuzia madini ili serikali iweze kukusanya kodi stahiki kwa maendeleo ya Taifa.